Home » » Kumbe Jaji Warioba alikuwa ‘mshereheshaji’?

Kumbe Jaji Warioba alikuwa ‘mshereheshaji’?

Written By Unknown on Jumapili, 13 Aprili 2014 | 02:52

WAKATI mchakato wa kuandaliwa kwa rasimu ya kwanza ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ulipoanza na kuwepo kwa rasimu ya pili iliyokabidhiwa kwa Rais Jakaya Kikwete ndipo nilipojua kuwa kazi aliyopewa  Jaji mstaafu Joseph Warioba haikuwa na tija ndani ya Bunge Maalumu la Katiba.
Kumbe Jaji Warioba na timu yake walipewa kazi ya kuongoza sherehe za Bunge Maalumu la Katiba na si kusherehekea Jubilei ya Muungano ambayo kwa tafsiri ya haraka wenye sherehe wanaendelea kufaidi matunda ya kuwemo ndani na mshereheshaji
akilipwa chake na kuondoka.
Nalazimika kuyaweka wazi mawazo yangu hivi leo baada ya kushitushwa na kebehi, kashfa, mzaha na kuandamwa moja kwa moja kunakofanywa na  wanasiasa ambao hawana mlengo mahususi unaopaswa kukubali na kuheshimu mawazo ya tume ya katiba iliyoundwa na rais mwenyewe.
Kibaya zaidi anayeandamwa sasa na zaidi ya wajumbe wote walioteuliwa na Rais Jakaya Kikwete kukusanya maoni ya wananchi na kuandaa rasimu ya kwanza na ya pili, nyongo sasa imepasukia kwenye moyo wa Jaji Warioba na si mwingine.
Jaji Warioba, mmoja wa waasisi wakongwe na kada mashuhuri wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) sasa amegeuka kuwa jiwe la pembeni lililokataliwa na waashi,  ambaye haonekani tena kwa dhamira yake na majukumu aliyopewa na rais ya kuiongoza tume ya katiba kuwa anautakia mema Muungano.
Jambo la ajabu na la kusikitisha, haieleweki ama Jaji Warioba alifanya kosa kwa kutokuwa na uelewa wa kutosha wa kukubali kuwasilisha mapendekezo yaliyoandikwa kwenye rasimu ya pili ya katiba kwa kutamka bayana kuwa kilichopendekezwa kwenye rasimu hiyo kilitokana na maoni ya wananchi waliohojiwa kuwa wanahitaji muundo wa serikali tatu ndani ya Muungano.
Kosa jingine ambalo pia inawezekana, jaji huyo msomi alilifanya labda hakueleweka sawa sawa kama yale aliyokuwa akiyasoma kabla ya Bunge Maalumu la Katiba halijazinduliwa na rais yalikuwa maoni yake binafsi ndiyo maana amezalisha uhasama mkubwa kutoka kwa Wana CCM chipukizi na wakongwe wenzake.
Ndiyo maana nathubutu kusema wazi kuwa kitendo cha aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Warioba kukubali au kushinikizwa kusoma  rasimu  ya pili ya katiba bungeni kabla bunge hilo halijazinduliwa na rais hilo lilikuwa kosa kubwa la kiufundi.
Inawezekana upotoshaji wa itifaki na intelijensia za kisiasa kulichangia kwa kiasi kikubwa kumfanya jaji huyo aonekana kama mwongoza sherehe za Bunge Maalumu la Katiba na haiba yake haikuonekana wazi kuwa alipewa heshima kubwa ya kuongoza kazi ngumu ya kuandaa rasimu hiyo.
Matokeo yake sasa mwanasheria huyo mkongwe, aliyewahi kuwa Makamu wa Rais na Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hapimwi tena kwa ukomavu wake wa kisiasa  ndani ya chama chake (CCM) na baadhi ya watendaji wa serikali alioweza kuwafundisha kazi, sasa anaonekana kuwa ni msaliti.
Kuwa mapendekezo yaliyowasilishwa na Jaji Warioba kabla ya bunge hilo kukamilisha kanuni zake na kuzinduliwa rasmi na rais kwa baraka zote kumempotezea heshima zaidi jaji huyo mstaafu kwa tabia na vitendo vinavyofanywa na vijana wadogo wa CCM kuwa kauli yake ya kuwepo kwa muundo wa serikali tatu ni donda ndugu ndani ya muungano.
Wameamua kumnyoshea vidole kila kukicha na kauli zinazotolewa na viongozi wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) kuwa chama chao hakikubaliani na mapendekezo ya serikali tatu yaliyowasilishwa na Jaji Warioba, wakionyesha kung’ang’aniza kabisa muundo wa serikali mbili zilizokuwepo tangu nchi mbili za Tanganyika na Zanzibar zilipoungana mwaka 1964.
Inawezekana dhana ya woga na upotoshaji inazidi kwa kasi kumuelemea Jaji Warioba na wengi wamesahau kuwa wajumbe wa tume ya katiba hawakujiteua wenyewe nao waliteuliwa vilevile na Rais Kikwete kwa kushirikiana na Rais wa Zanzibar, Dk. Mohamed Shein.
Kama walivyoteuliwa na marais hao na kupewa baraka, ofisi na vitendea kazi vyote muhimu wasingeliweza kuandika maoni yao kwa kushirikiana na sekretarieti iliyochaguliwa ili waweze kuchepusha mawazo ya wananchi na kuandika kwa kina mtazamo na mapendekezo yao.
Wajumbe 201 wa Bunge Maalumu  la Katiba nao leo hii wanaweza bila shaka wakawa wameingia kwenye mtego uliofanikisha kumnasa Jaji Warioba ili aonekane hadharani kuwa kazi aliyotumwa kuifanya alishindwa na ndiyo maana alikuja na mapendekezo ya muundo wa serikali tatu chini ya mwamvuli wa muungano.
Hayo yametokea lakini jambo la aibu na fedheha hata kabla Jaji Warioba hajapandishwa kwenye mimbali kusoma rasimu ya pili ya katiba, Bunge Maalumu la Katiba liligeuka kuwa uwanja wa fujo, vurugu na malumbano kuhusu upitishaji wa kanuni, aliyekuwa Mwenyekiti wa muda wa bunge hilo, Pandu Amir Kificho anajua kilichomkuta.
Kanuni ya 37 na 38 haikuweza kupitishwa hadi alipokuja kuchaguliwa Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta, vioja vya upigaji wa kura za ‘WAZI’ na ‘SIRI’ kulikochukua muda mrefu nako kuliweza kuutafuna muda wa bunge hilo kwani idadi ya siku zilizopangwa zilizidi kuyoyoma.
Hayo yote yametokea na mashuhuda  wa  kila aina ya hoja kutolewa, kuzomeana, kuomba mwongozo na kadhalika kumezidi kushamiri bungeni ilhali koti alilovaa Jaji Warioba likiendelea kutoteshwa ndani ya bunge hilo, hawa wanataka serikali mbili na hawa wanataka serikali tatu.
Jambo hili limegeuka kuwa kiini macho kwa kuwa kamati za Bunge Maalumu la Katiba zilizoundwa nazo zinakumbwa na jinamizi la theluthi mbili kukubaliana pale wanapohitaji kupitisha jambo, idadi hiyo kwa upande wa Tanzania Bara na upande wa Tanzania Visiwani (nchi ya Zanzibar).
Ndiyo maana naendelea kuiangalia kazi kubwa iliyofanywa na Jaji Warioba na timu yake ilifanana na mshereheshaji wa sherehe, mikutano au vikao (MC) ambaye hupatiwa kifuta jasho chake anapomaliza kazi na wenye mahitaji nao wanaendelea na kazi yao ya kuvunja kanuni.
Kama hayo yametokea na hali inazidi kuwa tete ndani ya Bunge Maalumu la Katiba sioni kama ilikuwepo haja  ya kuundwa kwa Tume ya Katiba iliyopewa dhamana  kubwa ya kuongozwa na jopo la wasomi, pia kuundwa kwa  Bunge Maalumu la Katiba kunazidi kuwaongezea wananchi simanzi kwa kuwa pesa za walipa kodi zote zinateketea ndani ya malumbano ya katiba mpya.
Jambo zito la kujiuliza iweje na nchi inashindwa kufikia kwenye malumbano ya staha na busara kama kile kilichojadiliwa na wananchi kikaonekana kinyume na fikra za watu wachache tu kwa sababu Watanzania wapatao 629 wamejaliwa kuwa na sauti za malaika na wengine zaidi ya milioni 45 wanaganga njaa uswahilini.
Basi niseme, kwa kuwa Jaji Warioba amevalishwa gunia la chawa, kwa kusoma rasimu ya pili ya katiba alipowasilisha mapendekezo yaliyoweka wazi na tume yake kuwa hayo ndiyo maoni  ya wananchi mshahara wake umebaki hobelahobela, kusimangwa, kupigwa vita, kutolewa kauli zisizokuwa na staha na pengine anastahili hivi sasa kunyang’anywa kadi ya CCM kwa kuwa hakubaliki na msimamo wa chama chake haumuungi mkono, pole Jaji Warioba.
Inawezekana kabisa kuwa hayo yote yanayoendelea kutokea hayakuwa matarajio ya Watanzania wengi kumuona Jaji Warioba akisulubiwa bila kosa kila kona, naamini hata Yesu Kristo au Nabii Issa alikutwa na kadhia zaidi ya hiyo wala asisononeke moyoni mwake bali awasamehe waliomteua na kumuamini.


Share this article :

Chapisha Maoni

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. bentabless.com - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger