Home » » CHADEMA kushindwa Chalinze ni funzo la tatu

CHADEMA kushindwa Chalinze ni funzo la tatu

Written By Unknown on Jumapili, 13 Aprili 2014 | 02:59

INGAWA ukweli wa haya nitakayoyaeleza ni PIGO jingine kwa CHADEMA, naomba nitumie neno FUNZO, labda viongozi wake watanielewa vizuri. ‘Funzo’ ni jambo au kitendo kinachomrekebisha mtu tabia.
Funzo la kwanza lilikuwa uchaguzi wa madiwani ambapo CCM kilizoa viti 24 na ‘kuwaachia’ CHADEMA viti vitatu tu.
Funzo la pili lilikuwa uchaguzi wa kiti cha ubunge Jimbo la Kalenga lililoachwa wazi kwa kifo cha aliyekuwa mbunge wake, William Mgimwa. Huko nako CHADEMA kilipigwa chini kwa mgombea wake kuangushwa na mwana wa marehemu aliyesimamishwa na CCM. Kweli maji hufuata mkondo.
Funzo la tatu ni uchaguzi wa mbunge wa jimbo la Chalinze ambalo pia lilikuwa wazi baada ya kifo cha aliyekuwa mbunge wake, marehemu Said Bwanamdogo. Aliyesimamishwa na CCM kugombea kiti hicho ni mwana wa Rais Jakaya Kikwete, aitwaye Ridhiwani. CHADEMA kilimsimamisha Mathayo Torongei aliyeangushwa kwa fedheha.
Wakati Ridhiwani akipata kura 20,828 sawa na asilimia 86.61, alimwacha kwa mbali Mathayo Torongei aliyepata kura 2,544 yaani asilimia 10.6. Mgombea Fabian Skauki wa CUF alipata kura 476, sawa na asilimia 1.98. Mgombea Ramadhani Mgaya wa AFP alipata kura 186 sawa na asilimia 0.59, huku Hussein Ramadhani wa NRA akiambulia kura 60, yaani asilimia 0.25.
Jimbo la Chalinze limekuwa chini ya himaya ya CCM tangu lilipoanzishwa mwaka 1995. Mbunge wake wa kwanza alikuwa Jakaya Mrisho Kikwete ambaye sasa ndiye Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anayekaribia kumaliza kipindi chake cha pili. Alifuatiwa na Ramadhani Maneno kisha Bwanamdogo aliyefariki dunia kabla ya kumaliza kipindi chake na sasa ni Ridhiwani Jakaya Mrisho Kikwete. Kama baba, mwana naye yu mumo humo.
Msimamizi wa uchaguzi huo, Samwel Sarianga, alisema waliojiandikisha kupiga kura walikuwa 92,000 lakini waliojitokeza kupiga kura walikuwa 24,422. Hii ina maana wapiga kura 67,578 waliojiandikisha hawakujitokeza kufanya zoezi hilo!
Soma walivyosema baadhi ya wananchi waliohojiwa baada ya uchaguzi wa Chalinze: “Tutaendelea kushiriki mikutano ya kampeni za vyama vitakavyokuwa vinatupatia chochote lakini hatutapiga kura kwani wote tuliowachagua katika jimbo letu hawajatuletea maendeleo!”
Bado viongozi wa CHADEMA hawajapata funzo kwa matokeo hayo? Hawajiulizi ni kwa nini idadi ya wapiga kura hupungua kila uchaguzi? Hawajiulizi ni kwa nini wapinzani (wakiongozwa na CHADEMA) hupata kura kiduchu vijijini na baadhi ya maeneo kutopata hata kura moja?
Mbele ya safari kuna uchaguzi wa wenyeviti wa serikali za mitaa baadaye mwaka huu (kama hautaahirishwa) na Uchaguzi Mkuu utakaofanyika mwezi Oktoba mwaka 2015. Wamejipanga vipi kushinda? Au ni yale yale ya kutosheka na wingi wa watu kwenye mikutano yao mijini huku wakiwa hawatambuliki vijijini? Si wote wanaohudhuria mikutano yao wamejiandikisha kupiga kura wala hawajui haki yao ya kufanya hivyo.
Mara kadhaa huko nyuma niliwaasa viongozi wa CHADEMA waangalie walikojikwaa badala ya kuangalia walikoangukia. Mtu mjinga huishia kujifunza kutokana na shida au taabu kwa sababu ya kupuuza ushauri. Hutumiwa kumwelezea mtu aliyepuuza ushauri aliopewa kisha akaishia kutumbukia katika matatizo mengi. Ni ufafanuzi wa methali ya “Fumbo la mjinga taabu.”
Viongozi wa CHADEMA wahamie vijijini kwa muda badala ya kukurupukia operesheni ya M4C ya mpito. Wapige kambi vijijini kuwapa wanavijiji elimu ya uraia, maana, umuhimu, faida za kujiandikisha na kupiga kura. Wawaeleze na kuwafafanulia maana ya upinzani ili kuwaondolea hofu kuwa ni watu wanaotaka kuleta machafuko nchini kama wanavyozugwa na CCM.
Tena kwa heshima na taadhima  naomba pia niwakumbushe methali isemayo: “Mtu haoni aibu yake huiona ya mwenziwe.” Kwa kawaida binadamu hawazioni kasoro zao ila huziona za wenzao. Huweza kutumiwa kwa mtu mwenye tabia ya kuwalaumu wenzake kutokana na aibu zao lakini hazioni zake mwenyewe.
Viongozi wa CHADEMA ndio waliokifanya CCM kitambue makosa yake kwani kimekuwa kikificha madhambi mengi ya serikali yake. Hili ndilo linalomzindua Katibu Mkuu wake, Abdulrahman Kinana, kukiri kuwa chama chake kitakuwa na wakati mgumu katika Uchaguzi  Mkuu mwaka 2015 kujibu maswali ya Watanzania kuhusu utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2010. Katika miaka ya hivi karibuni haikuwa rahisi kiongozi mkuu wa CCM kuikosoa serikali.
Maneno kama haya ambayo zamani yalikanushwa kwa nguvu na CCM, ndiyo yanayowapumbaza viongozi wa CHADEMA. Katika vita waweza kuwa na silaha nzito za kisasa kuliko mpinzani wako lakini kama huna utaalamu na mbinu ni bure.
CCM kina utaalamu na mbinu na ni wepesi wa kugeuza kibao dakika za ‘lala salama.’ CHADEMA bado hakijapata utaalamu na mbinu kama hizo!
CCM kinajivunia mfumo wake wa uongozi unaowashirikisha wajumbe wa nyumba kumi, mashina, matawi, kata, wilaya, mikoa mpaka makao makuu.
Kote huko makada wake hufanya mikutano kujadili mambo mbalimbali yanayohusu chama chao kuendelea kushika hatamu. Utokeapo uchaguzi wowote, makada hao hupita nyumba kwa nyumba usiku kuwahamasisha wananchi wawapigie kura wagombea wao.
Huko ndiko wanakowasihi wananchi ‘kutosikiliza na kubeza kelele na porojo za wapinzani, hususan CHADEMA.
Je, CHADEMA kina utaratibu kama huo huko vijijini? Au ni mpaka wakati wa uchaguzi ndipo kinapoonekana kwa mbwembwe nyingi na matumizi ya helikopta? Tuchukue mfano wa Dar es Salaam hususan Jimbo la Segerea. Uongozi wa juu unajua kinachoendelea miongoni mwa viongozi wa jimbo hilo?
Uongozi wa Jimbo la Segerea umegawanyika makundi mawili. Moja ni lile la viongozi  wanaokusudia kugombea udiwani na ubunge wa jimbo hilo kwa hali yoyote iwayo. Jingine linataka kukiimarisha chama kuanzia chini lakini linapigwa vita na hao wanaoutaka udiwani na ubunge kwa udi na uvumba.
Viongozi wa misingi na matawi wenye msimamo hawaalikwi kwenye mikutano ya jimbo wala viongozi wa jimbo hawatembelei misingi na matawi na hawajui yaliko! Uozo huu unajulikana makao makuu ya chama?
CHADEMA kitajengwa vipi kwa mtindo huu? Kama viongozi wa Segerea hawajui yaliko baadhi ya misingi na matawi chama kitakuwa na uhai?
Kama misingi na matawi yanabaguliwa kwa sababu viongozi wake ni wakweli wasiopenda unafiki, CHADEMA kisitegemee kulitwaa Jimbo la Segerea kirahisi kama inavyodhaniwa.
Viongozi wakuu wa CHADEMA wafanye hima kutembelea misingi na matawi ili waone jinsi uhai wa chama wa Jimbo la Segerea unavyopelekwa arijojo. Hili ni eneo moja tu mkoani Dar es Salaam bila kutaja maeneo mengine nchi nzima. Kama viongozi wa CHADEMA hawatazinduka sasa, nadhani hata viti walivyovitwaa kwenye uchaguzi wa mwaka 2010 watavipoteza.
Hali ikiwa hivyo viongozi wakuu watawaambia nini wananchi waliokuwa wakiimbishwa “people’s” nao kujibu “Power!”?
Viongozi wakuu wa CHADEMA wajiulize ni kwa nini hushindwa vijijini. Ndiko  kunakokinufaisha CCM kwani kimeeneza  mizizi yake huko.
Nimeeleza mwanzoni kuwa CCM ni fundi wa utaalamu na mbinu. Je, viongozi wakuu wa CHADEMA wana uhakika wa usafi wa nyumba yao? Wote wanakipenda CHADEMA kwa dhati? Hakuna mashushushu wa CCM wanaokidhoofisha bila wenyewe kujua?
Majuzi nilivutiwa na kipindi cha HOTMIX kinachorushwa na runinga ya EATV wakati mkazi anayeishi mpakani mwa Tanzania na Malawi alipouliza: “Serikali iliunda tume ya kupata maoni ya wananchi na ilitembea nchi nzima kwa ajili hiyo ikitumia fedha za wananchi.
Sasa kwa nini serikali hiyo hiyo inaacha maoni ya wananchi na kukazania ya kwake? Kulikuwa na sababu gani za kuunda tume kumbe serikali ilikuwa tayari ina msimamo wake?”


Share this article :

Chapisha Maoni

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. bentabless.com - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger