Home » » Bunge la Katiba mwenyezi Mungu alilaze mahali pema!

Bunge la Katiba mwenyezi Mungu alilaze mahali pema!

Written By Unknown on Jumanne, 29 Aprili 2014 | 23:53

RAIS wangu, koo langu limenikauka kama gae! Usiku na mchana nimekulilia wewe Bwana. Machozi yangu yamegeuka kuwa ndiyo chakula changu.
Kwanini unakaa mbali nyakati za shida? Taifa lako linaangamia, masikini wa nchi hii wanafanyiwa dhihaka na kusukumizwa kuzimu!
Waliopaswa kuwaongoza sasa wanajisalimisha kwa jeshi! Wamewatengenezea waja wako mazingira ya kumwaga da
mu kwa sababu tu ya ulevi wao wa madaraka!
Bunge Maalumu la Katiba lilikuwa ni mzaha aghali na wa aibu kubwa nchi hii haijapata kushuhudia katika historia yake. Umesema mwenyewe kuwa umekuwa ukifuatilia mchakato huo tangu ulipolizindua, lakini yaliyoendelea baada ya hapo yamekusononesha na kukusikitisha.
Bunge lilijaa kila aina ya uchafu. Matusi, maneno ya hovyo hovyo na lugha chafu zilizokuwa zinatolewa na baadhi ya wajumbe havikuacha tofauti yoyote na yale tunayoyaona kwa walevi tunaokutana nao tunapokatisha kwenye vilabu vyao vya pombe za kienyeji!
Ulipokuja kukaririwa tena na chombo cha habari kuwa ukiliangalia kwa undani linakufurahisha, unawapa wakati mgumu sana waliotaka kukutenganisha na uchafu huu.
Si kawaida aibu kumfurahisha mtu makini! Madhali sasa Bunge la Katiba limekoma, tumwombe Mwenyezi Mungu alilaze mahali pema, na wajumbe wake wakapumzike kwa amani hadi ukomo wa utawala huu!
Rais wangu, wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na wabunge wa Bunge la Jamhuri hawakuchaguliwa na wananchi kuwa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba. Na hawa ndio wamekuwa kiini cha fujo na mambo ya aibu.
Hali hii ndiyo iliyosababisha Bunge kuwa na hawa wengi na hawa wachache. Hili lilikuwa kosa kubwa. Hii ni hila iliyofanywa bila watetezi wa wananchi kuigundua.
Kwakuwa mchakato huu uliuanzisha wewe binafsi, ungefanikisha ungetuzwa kwa haki na wala si kwa vijisifa vya kufedhehesha vitengenezwavyo na wanadamu.
Nawe ukishapita jina lako lingeenziwa na vizazi vingi vijavyo. Huja hukutambua kuwa ulichoanzisha kilikuwa sawa na safari ya majini. Kama hujui kuogelea, hata wimbi dogo tu linakubeba.
Baba, katika hili nia yako njema imebebwa na mawimbi. Matumaini ya Watanzania kupata katiba bora chini ya uongozi wako umeyafifisha mwenyewe! Madhali sasa Bunge la Katiba limekoma, tumwombe Mwenyezi Mungu alilaze mahali pema, na wajumbe wake wakapumzike kwa amani hadi ukomo wa utawala huu!
Rais wangu, wananchi wamefarijika kwa habari kuwa jumuiya na taasisi za Kiislamu Tanzania zimeungana na maaskofu mbalimbali kuwataka wajumbe wa Bunge la Katiba kuheshimu rasimu ya katiba iliyowasilishwa kwa
mujibu wa sheria na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Viongozi wa dini ambao bado hawajachakachuliwa na wanasiasa bado wapo! Tuendelee kuwasikiliza. Wanaotutaka tuwaombee walevi hawa badala ya kuwakanya waache ulevi wamechakachuliwa!
Tuwapuuze bila kujali vyeo vyao katika dini wanazoziongoza! Walevi wanaombewa? Maoni ya wananchi kama yalivyokusanywa na tume ni sauti ya Mungu mwenyewe, lazima yaheshimiwe na wote.
Wenye hila ya kutaka kuyapindisha laana ya Mungu wetu na iwe juu ya kichwa chake na juu ya nyumba yake! Kama Samuel Sitta alidhani Muadhama Polycarp Kardinali Pengo na Sheikh Mkuu Mufti Shaban bin Simba ndio pekee wa kusikilizwa, alikuwa anajidanganya mwenyewe! Muda wake wa kutumika hata ki-hila umekwisha.
Rais wangu, walioendelea na Bunge baada ya wengine kususa walikuwa wahuni. Waliacha kujadili rasimu wakawa wanajadili watu waliotoka.
Upunguani huu ulisababisha wananchi kudhulumiwa kiasi kikubwa cha fedha, laki tatu kila siku! Wahuni wa aina hii wanastahili kabisa kudharauliwa na kila mwenye mapenzi mema na nchi hii! Wanaodhani wanaweza kufanikisha katiba mpya kwa hila, hawajui kuwa kwakufanya hivyo, wanakupatiliza wewe baba uliyeanzisha mchakato mzima!
Wanataka wananchi wadhani ulianzisha kitu ambacho ulikuwa hujui ukubwa wake. Kuiingiza nchi katika zahama kubwa kama hii lazima uwajibike!
Wakati huo ukifika, baba hao wasaka tonge hutamwona hata mmoja! Utakuwa peke yako! Ndipo maneno ya mwanamwema Alto Makombwe wa Geita yatakapotimia.
Alisema: “Lakini kwa sababu wewe unaandika ukweli siku itafika utaenziwa na kutuzwa!” Ndugu Rais, madhali sasa Bunge la Katiba limekoma, tumwombe Mwenyezi Mungu alilaze mahali pema, na wajumbe wake wakapumzike kwa amani mpaka ukomo wa utawala huu!
Kingunge mkana dini, mwana wa aliyekuwa Katekista wa Kanisa Katoliki kule Kilwa Kipatimu enzi zile, marehemu Ngombale Mwilu kaibuka kutoka katika kundi la waganga wa kienyeji na kusema kuwa Bunge Maalumu la Katiba limekuwa ni mateso kwani lugha za matusi na kuzomea viliwadhalilisha mbele ya wananchi!
Anachoshangaza Kingunge ni kutoa kauli hiyo siku ya mwisho. Tangu mwanzo lugha hizo ndizo zilizokuwa zinatawala, alikuwa wapi?
Pamoja na kupewa nafasi nyingi hakukemea hali hiyo hata mara moja. Wala hakumkanya Mwenyekiti wa Bunge hilo asiendelee kushabikia hali hiyo kizuzu kama wengine. Ameshuhudia Baba Warioba na wenzake wakikashifiwa na kutukanwa tangu mwanzo hadi mwisho.
Leo ndiyo anasema waliomkashifu Warioba ni wapuuzi waliokengeuka. Muda wake wa matumizi hata ki-hila
umekwisha!
Rais wangu, zamani mvi zilikuwa ni ishara ya busara! Kwa mvi zake na za Mwenyekiti wa Bunge na wengine wengi waliokuwamo humo, wananchi hawakutegemea wafikishwe hapa walipofikishwa!
Wenye kutukana na wenye lugha za hovyo hovyo wengi walikuwa ni vijana ambao walidhani matusi yangeweza kujazia uwazi mkubwa uliomo ndani ya vichwa vyao.
Walipotoka waliotoka ndipo ikajulikana walevi walikuwa ni akina nani.
Wakaonekana wakielea kama mafuta yaeleavyo juu ya maji! Badala ya kujadili rasimu wakawa wanajadili serikali tatu. Hawakujadili serikali mbili, lakini wenye upungufu mkubwa walikiri ujinga wao hadharani kwa kumalizia kuwa: “Mimi ni muumini wa serikali mbili!
Waliowaomba waliotoka warudi kwa kuwatukana waliwathibitishia wananchi ujinga wao bila kuacha shaka yoyote! Sauti za wajinga zilisikika zikisema: “Wasuse wasisuse katiba lazima itapatikana.” Mjinga zaidi yao akasema ataingia msituni!
Naye mwana wa shetani akamkumbuka baba yake kwa kudhani kuwa waliosusa walikuwa ni baba zake wadogo, akawaita shetani jina la baba yake.
Katiba ni maridhiano! Itakuwa ni katiba ya aina gani hiyo itakayopatikana bila maridhiano? Upumbavu ni kilema, ujinga una nafuu!
Kwa muda wote huo na pesa zote hizo wamejadili sura mbili tu, nazo kipengele kimoja kimoja tu ambavyo hata navyo havijaeleweka wameafikiana nini.
Hawa ndio viongozi wetu! Sijui ni mikosi gani tulizaliwa nayo! Ndugu Rais, madhali sasa Bunge la Katiba limekoma tumwombe Mwenyezi Mungu alilaze mahali pema, na wajumbe wake wakapumzike kwa amani hadi ukomo wa utawala huu!
Rais wangu, mwanamwema Robbie Natai akanitumia ujumbe akisema: “Mwalimu, hebu niulizie hawa watu waliopo Dodoma maana Watanzania wengi tunawashangaa na zaidi ya yote tunapata machungu moyoni.
Wajumbe hao wanaikataa rasimu iliyowasilishwa na Baba Warioba, sasa wanajadili rasimu ipi?”
Naye Leonard kutoka Kigoma akaniandikia: “Mwalimu, hawa watu hawana uchungu na sisi! Kwao katiba ni ile ya ulinzi wa madaraka yao. Kama walikuwa na rasimu yao, ni kwanini wanateketeza pesa zetu? Si waandike hayo wanayoyataka waondoke huko Dodoma? Wana bahati wanawatawala watu wapole au niseme wajinga! Kwanini tusitoke wapenda nchi wote tukawafurushe tuokoe fedha zetu? Mimi nafurahia mafundisho yako ya kila Jumatano. Mungu akubariki sana.”
Rais wangu, Bunge unalosema linakufurahisha limekoma, lakini haya ndiyo machungu lililowaachia wananchi. Nani mwenye mapenzi mema na nchi hii atalitamani au kumtamani muasisi wake?
Pepo mchafu ameingia nchini mwetu! Madhali sasa Bunge la Katiba limekoma, tumwombe Mwenyezi Mungu alilaze mahali pema, na wajumbe wake wakapumzike kwa amani hadi ukomo wa utawala huu! Upuuzi mwingine sasa basi!


Share this article :

Chapisha Maoni

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. bentabless.com - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger