Home » , » Kijana anapokata tamaa hupoteza ndoto yake

Kijana anapokata tamaa hupoteza ndoto yake

Written By Unknown on Alhamisi, 1 Mei 2014 | 13:39

KATIKA maisha ya kila siku tunahimizwa kuwa tukipata tufurahi na tukikosa tutafakari.
Kushindwa kunafananishwa na giza linalotangulia mbele ya mwanga wa kushinda, ambapo ndiyo mafanikio yenyewe yalipo.
Juhudi kubwa ni kupambana na hilo giza ili kufanikiwa kwa kujifunza, kushindana na kushinda kwa kuwa hakuna mshindi pasipo mashindano.
Njia ya uhakika ya kutokushindwa ni kudhamiria kushinda. Ni wazi kuwa jinsi unavyofikiria ndivyo
utakavyokuwa kama msemo usemao: “Penye nia pana njia.”
Tatizo kubwa linalosababisha watu wengi kutoyafikia mafanikio yao ni kukata tamaa.
Wengine huhisi kuwa wamepita njia ambayo haijawafikisha kwenye malengo yao, jambo linalosababisha msongo wa mawazo na wengine kuchanganyikiwa na kujikuta wakiongea wenyewe barabarani.
Kukata tamaa kunaleta uvivu wa kutojishughulisha katika mambo ya kukuletea maendeleo, jambo linaloweza kumfanya mtu kuwa tegemezi.
“Matumizi mabaya ya fedha ujanani na kutojiwekea akiba ni maandalizi mabaya ya uzeeni,” huu ni msemo unaotumika kuwahamasisha vijana na wenye umri wa makamo kufanya kazi kwa bidii na kujiwekea akiba kwa ajili ya maisha yajayo kwani maisha fainali uzeeni.
Unapokata tamaa jiulize nani anayejali? Jibu ni hakuna anayejali, hivyo cha msingi simama na uyashinde maisha.
Itumie fursa uliyonayo katika maisha yako. ‘Ukipiga picha’ ya kushindwa katika jambo lolote unalotaka kufanya ujue unaelekea kushindwa.
Piga picha ya mafanikio utashinda na amini kuwa umezaliwa kushindana si kushindwa. Jaribu kufanya kitu kizuri unaweza kufanikiwa.
“Siku zote usifanye kitu kibaya ili upate kitu kizuri, bali fanya kitu kizuri ili upate kitu kizuri zaidi,” hayo ni maneno ya mwimbaji Mwasiti Almasi.
Wapo wanaoamini kuwa mafanikio huletwa na bidii katika kazi na wengine huamini kuwa mafanikio ni majaliwa.
Katika maisha ya kila siku unaweza ukawa umeshakutana na watu wanaoyashangaa maisha yao, wanashangaa kwa sababu walikubali majaliwa yaliyowapeleka kwenye  mafanikio.
Mafanikio katika maisha yanaanzia kwenye mitazamo na fikra zilizoko ndani ya mtu, kile kilichoko ndani ya mtu ndicho kitakachomhesabia mafanikio yake.
Mtazamo pekee ndio msingi wa maisha kwa kuwa unachukua asilimia 64 ya nafasi katika maisha ya mtu.
Ni vema tukajifunza kutengeneza mitazamo chanya ili tuweze kufanikiwa na njia mojawapo ya kutengeneza ni kufikiria mema tu na kuacha kufikiria mabaya kwa sababu siri ya kushinda katika maisha ni kuondoa fikra za kushindwa.
“ Mtu mmoja alikuwa akiishi kwa kuuza maputo ya rangi nyekundu, njano, kijani na bluu. Aliyaweka nje ya duka yakiwa yanapaa juu angani, watoto wengi walivutiwa na kuyanunua.
“Mauzo yake yakapanda juu sana, siku moja akaja mtoto mdogo na kumuuliza yule muuzaji kuwa endapo angekuwa na puto la rangi nyeusi nalo lingeweza kupaa angani.
“Muuzaji akamjibu kinachofanya puto lipae angani si rangi yake bali kile kilichomo ndani…hivyo kinachotufanya sisi tuwe juu ni mtazamo tulionao,” kinaeleza kitabu cha You Can Win kilichoandikwa na Shiv Khera.
Umewahi kujiuliza kwanini watu au kampuni nyingine zina mafanikio kuliko nyingine?
Hii  si siri, hawa watu wanafikiri na kufanya kazi vizuri, wamejifunza jinsi ya kuwekeza kwa watu wenye mitazamo chanya. Mafanikio ya mtu, kampuni au nchi yanategemea sana ubora wa watu wake.
Mfano kuna mnara mrefu,  maarufu kama Calgary Tower wenye urefu wa mita 190.8 na uzito wa tani 10,884; ambapo tani 6,349 iko chini ya ardhi ambayo ni sawa na asilimia 60 ya jengo zima.
Hii ina maanisha kwamba majengo marefu duniani yana misingi imara hata karibia uzito wa robo tatu ya jengo zima.
Kama iliyo kwa mnara mrefu na mzuri duniani ulivyo na msingi imara, vivyo hivyo hata kwa binadamu yeyote anapaswa kuwa na msingi imara.
Kitabu cha ‘You Can Win’ kinaeleza kwamba mkulima mmoja wa Afrika alikuwa na shamba kubwa na bado alikuwa na maisha duni.
Siku moja akaja mtu mwenye busara nyumbani kwake akamwambia kuwa iwapo mkulima huyo angepata almasi yenye ukubwa sawa na kichwa chake angekuwa tajiri mpaka kufa kwake na watoto wake.
Huyo aliposikia hivyo haikupita muda akauza shamba lake lote akasafiri kwenda nchi za nje na familia yake kuitafuta almasi na kuinunua.
Alipofika huko akakuta pesa aliyokuwa nayo ni ndogo haiwezi kununua almasi na alishaitumia kama nusu hivi kwa gharama za kusafiria, kwa  mawazo akaamua kujiua kwa kujitupa kwenye mto.
Baada ya muda mfupi yule mtu aliyeuziwa lile shamba akagundua kuwa kwenye shamba lile kulikuwa na mawe yanayong’aa akayachukua kwenda kupima akakuta ni almasi akayauza na kuwa tajiri.
Yule mtu mwenye busara aliposikia habari hizo akaamua kwenda kumtembelea yule mkulima alipofika kwenye lile shamba akamuulizia akaambiwa kuwa mkulima huyo alishaliuza shamba hilo kwa mtu mwingine na akasafiri kuelekea mbali, yule mtu mwenye busara akasikitika sana.
Hadithi hii ya mkulima ina maana kuu tatu; kwanza mtazamo wako unapokuwa sawa,utagundua kwamba unatembea kwenye fursa, hivyo hatuhitaji kwenda popote kinachotakiwa ni kugundua nafasi hizo.
Pili; wakati unaposifia uzuri wa majani ya upande wa watu wengine ujue kuna watu wengi wanayakubali majani yaliyopo upande wako na wanatamani hata kufanya kazi na wewe, lakini kwa sababu hauzingatii majani ya shamba lako unachukua muda mwingi kuangalia majani ya shamba la mwenzako, hivyo unaweza kufa maskini usipokuwa makini.
Tatu; bahati haiji mara mbili kwenye maisha, inayofuata inaweza ikawa nzuri zaidi au mbaya, lakini kamwe haiwezi kujirudia, tambua hilo, watu wengi wanashindwa kutambua bahati zao na fursa hata itakapobisha hodi au kuonyesha dalili.
Mitazamo yetu huwa inaonyesha wazi ni nini tulichopanga kukifanya, kwa wenye mtazamo chanya inaweza kuwa ni jiwe la mafanikio lakini wenye mitazamo hasi inawezekana likawa tofali.
Kampuni kubwa hazipimwi kwa kiwango cha fedha walichonacho bali wanapimwa kwa mtazamo wao na ushirikiano wao na jinsi ambavyo wafanyakazi katika kampuni hiyo wanavyojihisi wakati wanafanya kazi.
Mfano, mwekezaji anaposema kuwa: ‘Siwezi kufanya hiki,’ kuna maana mbili; moja ni kwamba hajui jinsi ya kufanya hicho kitu, pili, hataki kufanya hicho kitu.

Kama hajui jinsi ya kufanya hicho kitu basi hilo ni jambo la kukosa ujuzi na kama hataki basi shida iko kwenye mtazamo kwa maana ya kwamba hajali thamani ya hicho kitu. Hivyo tukubali kubadilika katika mitazamo chanya.
Share this article :

Chapisha Maoni

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. bentabless.com - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger