Home » » Sitta alizungumza nini na viongozi wa dini??

Sitta alizungumza nini na viongozi wa dini??

Written By Unknown on Alhamisi, 17 Aprili 2014 | 02:23

RAIS wangu, siku chache zilizopita, Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta aliwatembelea viongozi wawili wa dini,
Muadhama Polycarp Kardinali Pengo na Sheikh Mkuu wa Tanzania Mufti Shaban bin Issa Simba.
Yaonekana viongozi hawa wawili kwake ndio viongozi wa dini wa muhimu zaidi. Ni kweli kuwa wana waumini wengi zaidi. Ukiwarubuni utawapata maamuma wengi.

Hakuwakumbuka hata viongozi wa dini maswahiba wake waliokuwa wanamruhusu kuyatumia makanisa yao kama majukwaa ya kulialia juu ya mahasimu wake katika kufanya ufisadi. Maongezi yao yalikuwa ya siri.
Dunia imezoea kuona mambo yote ya kishetani kufanywa gizani, huku yakigubikwa na usiri mkubwa! Mambo yanayompendeza Mungu hufanywa kwa uwazi.
Sitta akitabasamu anasema alikwenda kuwajulisha yanayotokea bungeni. Ah! Ni Mtanzania gani ambaye haoni na kusikia utoto, upuuzi na mambo ya aibu yanayotokea bungeni?
Hadi wanatamani wajumbe wake ndio wangekuwa abiria wa ndege ya Malaysia, wakazame baharini! Hawa watakuwa viongozi gani ambao Sitta anataka kusema hawauoni ufedhuli unaotokea bungeni hadi akawaeleze?
Rais wangu, madhali Sitta ameshindwa kuwaambia wananchi kile alichowaeleza viongozi wa dini, basi viongozi hao wawaambie waumini wao na wananchi kwa jumla ni nini Sitta aliwaambia.
Wasipofanya hivyo heshima yao katika jamii itakuwa shakani. Timamu watawaweka kundi moja na Sitta.
Rais wangu, Samuel Sitta kama Adamu na Hawa walivyokula tunda walilokatazwa na Mwenyezi Mungu na hivyo wakaifanya dunia kuwa mahali pa mateso hadi mwisho wa dunia, ndivyo alivyoifanya nchi hii kuwa mahali pa mateso hadi leo kwa kupotosha hoja ya Richmond.
Waliwahukumu ambao hawakustahili kuhukumiwa na wakawahifadhi waliostahili kuhukumiwa! Kuzuga wakazuka manabii wa uongo waliohubiri kupandikiza chuki na fitina kati ya watu wa Mungu waliokuwa wamezoea kuishi kwa upendo, amani na mshikamano.
Miaka miwili mfululizo makamanda wa kishetani waliopanda majukwaani kuhubiri ufisadi wao, hakuna hata siku moja waliosikika wakihubiri neno la amani, upendo na mshikamano miongoni mwa Watanzania. Waliendelea kulialia hadi walipotunukiwa.
Kwa bahati mbaya masikini wa nchi hii waliwasikiliza wana hawa wa shetani bila kugundua unafiki wao. Leo Sitta hata malipo ya Dowans yamekuwa kama halali!
Nalikumbuka vizuri sasa gazeti makini la MwanaHalisi. Liliandika kwa herufi kubwa, Sitta umeifunga kihuni hoja ya Richmond bungeni, lakini kwa wananchi hoja ya Richmond haitafungwa!
Uhuni uliofanywa katika kuimaliza hoja ya Richmond bungeni, ndio uliowaletea magumu masikini wa nchi hii hadi leo, Masikini wa nchi hii wataendelea na maumivu ya Richmond hadi watakapoamka kifikra na kuwaweka kikaangoni Sitta na wenzake ili wauseme ukweli waliouficha. Ana deni kubwa mtu huyu kwa masikini wa nchi hii.
Rais wangu, Samuel Sitta amepoteza fursa ya pekee alipokutana na viongozi wakuu wa dini. Kwa kuwa umri wake umekwenda, angeitumia fursa hiyo kutubu mbele yao na mbele ya Mwenyezi Mungu amsamehe kwa aliyoifanyia nchi hii siyo kuongeza mengine.
Baba Muadhama Polycarp Kardinali Pengo naye akumbuke kuwa kauli ya kejeli ya ‘chaguo la Mungu’ ilianzia kanisani kwake, nayo bado inakera waumini wake hadi leo. Asiongeze na hili.
Kufanya siri na watu wa aina hii kunaongeza shaka na kuliumiza Kanisa la Mungu. Kanisa likiungana na watawala na kuwaacha kondoo wa Bwana bila mchungaji mwema, Mungu hatakubali.
Atamtuma Baba Joseph Sinde Warioba na wenzake kuwachunga hata kama hawatakuwa na fimbo ya kichungaji.
Tume aliyokuwa anaiongoza Baba Warioba ni Tume ya Rais. Ndiyo kusema maoni ya wananchi yaliyokusanywa na Tume ya Rais, yalikusanywa na rais mwenyewe.
Kwa kuwasilisha maoni ya watu wa Mungu kama walivyoyatoa, Baba Joseph Sinde Warioba amejipatia thawabu kubwa mbele ya Mwenyezi Mungu.
Thawabu ambayo angeistahili muanzilishi. Lakini kama Waswahili wasemavyo, “Mwenyezi Mungu hamfichi mnafiki”, mwenyewe kaikana!
Viongozi hawa wa dini, waliishakaririwa wakishabikia serikali mbili kama CCM wanavyoshabikia.
Lakini nao kama CCM, hawasemi serikali mbili katika nchi moja kama zilivyoachwa na waasisi wa Muungano Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Abeid Amani Karume.
Hawana ujasiri wa kuwaambia watawala waifute nchi ya pili iliyojitokeza baada ya waasisi kufa ili kuondoa utata. Wanatamani kuunganisha nchi mbili kwa serikali mbili, kitu ambacho hata Nyerere na Karume hawakuweza.
Kutamani tu kuunganisha nchi mbili kwa serikali mbili, wanasema kunaonyesha kama vile umeme unaoingia kichwani ni mdogo.
Rais wangu, nawaomba waumini wa dini zote, wanapowaona viongozi wao wa dini wanaambatana na wanasiasa wachovu, waliopauka kisiasa kwa tamaa, wao wasiiharibu imani waliyonayo kwa Mungu wao.
Waendelee kuamini kuwa Mwenyezi Mungu yupo. Na sisi wote tunaomtumikia ni stahili yetu kuitwa watumishi wa Mungu. Hakuna mwenye haki ya kudai kuwa yeye ndiye mtumishi wa Mungu zaidi.
Kuwa kiongozi wa dini ni mpango wa Mungu tu kuwa kila palipo na kundi kuwe na kiongozi. Ndiyo maana tuna viongozi wa vikundi vya kisiasa, vya kiharakati na hata vya kigaidi.
Wanyama nao hata siafu wana viongozi wao! Mwenyezi Mungu hana balozi wa kumwakilisha hapa duniani. Toka manabii na mitume wapite hajamtuma mtu duniani kuja kumwakilisha.
Rais wangu, kama viongozi hawa hawawezi kuwaambia waumini wao kile walichoambiwa na Sitta, basi wawaambie nini wao walimwambia Sitta. Je, walimtaka awaeleze ilikuwaje Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Jaji mstaafu Joseph Sinde Warioba awasilishe rasimu kabla Bunge halijawa?
Kamusi ya Kiswahili sanifu kama ilivyochapishwa na Oxford inatafsiri neno ‘zindua’ kuwa ni ‘anzisha’ au ‘fungua kitu kwa mara ya
kwanza ili kianze kutumika’.
Hivyo kabla ya kuanzishwa (kuzinduliwa) na rais, hapakuwapo na Bunge la Katiba. Baba Warioba alilazimishwa kuwasilisha rasimu kwa kikundi tu cha watu ambao wahuni wachache wamefanikiwa kulifanya kundi lote lionekane kama la wahuni tu.
Rasimu inayojadiliwa haijawasilishwa rasmi bungeni! Huu ni uhuni. Je, ndiyo huu uhuni waliokuja kujulishwa viongozi wetu wa dini? Lakini je, walimkanya asichakachue maoni ya wananchi kwenye rasimu?
Rais wangu, achana na wanasiasa hawa ambao muda wao wa kutumika umekwisha. Mikakati wanayoifanya inawaongezea hasira tu wananchi.

Busara sasa ni wewe kumsikiliza Katibu Mkuu wako Abdulrahman Kinana kule vijijini anakohangaika na shida za masikini wako. Anajenga, hawa wanabomoa! Siku za hukumu zinakuja, hawa hutawaona!
Share this article :

Chapisha Maoni

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. bentabless.com - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger