Home » » Ngeleja awaita UKAWA mezani

Ngeleja awaita UKAWA mezani

Written By Unknown on Jumatano, 30 Aprili 2014 | 00:17

SUKU moja baada ya vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) kueleza kusudio lao la kufungua kesi Mahakama Kuu kuhoji mamlaka ya Bunge Maalumu la Katiba, Mwenyekiti Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala, William Ngeleja, amewataka kurudi kwenye
meza ya majadiliano ili kupata muafaka.
Akizungumza na Tanzania Daima jana katika viwanja vya ofisi ndogo za Bunge, Ngeleja alisema kuwa suala la UKAWA kutoka nje si jambo jema na kuwataka warejee ili watunge katiba ya wananchi.
Ngeleja ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati Na. 9 ya Bunge Maalumu la Katiba, alisema kuwa UKAWA kuendelea kuwa nje ni kutowatendea haki wananchi ambao wana kiu ya mabadiliko ya katiba yao.
Akijibu swali lililomtaka kueleza hatua iliyochukuliwa na UKAWA ya kwenda mahakamani, Ngeleja alisema kuwa sheria iko wazi na hawazuiwi ili wakapate ufafanuzi wa kisheria.
Akizungumzia utata wa kupatikana theluthi mbili ya kura kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, Ngeleja alisema kuwa Bunge Maalumu la Katiba lina mamlaka kamili na sheria namba 83 ipo wazi.
“Sheria inaeleza mamlaka ya Bunge Maalumu la Katiba yaliyotajwa katika kifungu cha 25 cha sura hiyo ambayo yanaruhusu mamlaka ya Bunge kujadili na kupitisha masharti ya katiba yanayopendekeza mpito wa masharti mengine kama Bunge hilo litakavyoona.
“Kifungu namba 26 (1) kinalipa Bunge Maalumu la Katiba uwezo wa kutunga kanuni kwa ajili ya kuendesha Bunge hilo, kutokana na mamlaka kanuni zilitungwa na Bunge Maalumu la Katiba kusaidia kuendesha mjadala wa katiba mpya,” alisema.
Alisema kuwa kutokana na mamlaka, Bunge la Katiba lina uhalali wa kuweza kujadili, kurekebisha, kubadili na kuondoa mapendekezo yoyote yaliyomo katika rasimu ya katiba.
Aliongeza kuwa uwepo au kutokuwepo kwa UKAWA katika Bunge hilo linalotarajiwa kurejea Agosti mwaka huu, hauthibitishi kupatikana kwa theluthi mbili.
Ngeleja alitamba kuwa kamati yake ilifanikiwa kuongoza makubaliano yote katika kupata theluthi mbili bila kujali tofauti za makundi.


Share this article :

Chapisha Maoni

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. bentabless.com - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger