Home » » Lukuvi maji shingoni

Lukuvi maji shingoni

Written By Unknown on Jumatatu, 28 Aprili 2014 | 04:11

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Urataibu wa Bunge), William Lukuvi, amezidi kukaliwa kooni kwa kutakiwa kujiuzulu kwa madai ya kutoa kauli za uchochezi kanisani.
Msimamo huo ambao ni wa pili kutolewa dhidi ya waziri huyo, ulitolewa jana katika Msikiti wa Mtambani jijini Dar es Salaam  wakati wa ufunguzi wa kongamano la Jumuiya
na Taasisi za Kiislamu zenye msimamo  mkali.
Mbali ya kujadili kauli ya Lukuvi, kongamano hilo pia lilijadili umuhimu wa kufanya maboresho kwenye daftari la kudumu la wapiga kura, ambalo wanadai limekuwa likiwaacha nje baadhi ya vijana wa Kislamu waliofikia umri wa kujiandikisha kupiga kura.
Kongamano hilo liliwakutanisha watoa mada mashuhuri,  wakiwemo maimamu wa misikiti mbalimbali kutoka Tanzania Bara na Visiwani.
Akizungumza kwa niaba ya viongozi hao, Msemaji wa Taasisi hiyo, Sheikh Rajabu Katimba, alisema lengo la kukutana na wanajumuiya hizo ni kufanya maazimio ya pamoja juu ya kauli za uchochezi zilizotolewa na Lukuvi pamoja kujadili daftari la kudumu la wapiga kura.
“Bado tunaendelea na msimamo wetu juu ya mchochezi huyo anayetaka kuvuruga amani, hatutaishia kwenye kongamano hili, tutafanya nchi nzima na kutoa uelewa kwa Waislamu na Watanzania wapate kujua madudu aliyosema Lukuvi,” alisema Katimba.
Alisema licha ya kusambaza nakala kwa viongozi wakubwa wa nchi na Watanzania, wataendelea kulaani kauli ya Lukuvi hadi Rais Kikwete atakapoamua kumwajibisha.
“Kauli za Lukuvi hazivumiliki kwani ni hatari kwa taifa, kiongozi mkubwa  kuongea vitu kama vile haifai,  tena badala ya kwenda bungeni kuomba radhi kwa Waislamu na Watanzania, yeye kazidi kuonyesha uhodari wa kuchochea uvunjifu wa amani,”  alisema Katimba.
Aliongeza kuwa wamekuwa na utaratibu wa kufanya makongamano mara kwa mara ili kutoa elimu zaidi kwa Waislamu,  pamoja na kujadili mchakato wa katiba na sio kwa Mkoa wa Dar es Salaam bali watahakikisha wanazunguka  nchi nzima kutoa elimu hiyo.
“Hatujasitisha makongamano, tutaendelea kama kawaida mpaka tutakapopata muafaka juu ya kiongozi  huyo, la sivyo tutazidi kuongeza kasi ya kuwafikia Waislamu na Watanzania popote pale walipo, na wakati huo tukifanya utaratibu wa kuchukua hatua  za kisheria,” alisema.
Kuhusu daftari la kudumu la wapiga kura, Sheikh Katimba alisema liboreshwe kwani kuna vijana wa Kiislamu waliotimiza umri wa miaka 18 mwaka 2014 na wengine mwaka 2013, lakini hawamo kwenye orodha ya wapiga kura.
“Endapo vijana wetu waliotimiza umri huo wa kupiga kura wasipoandikishwa kwenye  daftari  hilo, hatutokubali na tutakuwa tayari kwa lolote lile mpaka kieleweke, pia tutasimamia haki yao hadi ipatikane, kwani kuna vijana wetu wengi wanaachwa na kukosa haki zao za msingi kumchagua kiongozi wanayemtaka,” alisema.
Aliilaumu serikali kwamba imekuwa haizingatii kutenda haki kwa Waislamu katika masuala ya elimu.
“Tunaminywa haki zetu Waislamu, Mahakama ya Kadhi imetupiliwa mbali, hata katika masuala ya kiuchumi bado tunasumbuliwa, hasa kwenye Umoja wa Kiislamu (OIC), kwa mfumo huo hatutakubali na tutadai haki zetu hadi kieleweke kupitia makongamano haya,” alisema Katimba.
Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kiislamu na Mihadhara Zanzibar ya Uamsho, Abdallah Said Ally,   ambaye alikuwepo katika Msikiti wa Mtambani jana, alisisitiza kauli waliyoitoa hivi karibuni ya kumtaka Lukuvi kuachia ngazi.
Kuhusu Muungano
Akizungumza katika kongamano hilo, Sheikh Ali Baseleh, amesema kuwa mamadiliko ya katiba lazima yafanyike kwa sababu ya katiba ya sasa ina kasoro kubwa katika muundo wa Muungano.
Sheikh Baseleh, alisema sio kweli kuwa waliopendekeza na wanaounga mkono muundo wa serikali tatu, wanataka kuvunja Muungano.
“Kama maoni ya wananchi kuhusu serikali tatu yalikuwa hayatakiwi, kwanini zimetumika pesa nyingi kuunda tume ili ishughulikie suala la katiba mpya?” alihoji.
Alisema wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, walipaswa kujadili maoni ya wananchi yaliyomo kwenye rasimu, lakini waliyaacha na badala yake walikuwa wakipeana mipasho na kudhalilishana na hadi lilipoahirishwa, hakuna jambo la maana lililokwishafanyika.
“Haya maoni ya wananchi yameletwa kwa ajili ya kuboresha katiba kwa sababu ya sasa ina kasoro nyingi, leo Chama Cha Mapinduzi (CCM) hawataki, wanataka kuleta maoni yao ya serikali mbili ambayo hayamo kwenye rasimu,” alisema.


Share this article :

Chapisha Maoni

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. bentabless.com - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger